Jumatano, 3 Agosti 2016

MIL. 200/- ZA MBUNGE MTAJI KWA WAJASIRIAMALI MUSOMA







WANAWAKE katika Manispaa ya Musoma mkoani Mara wamepata mikopo yenye thamani ya Sh milioni 200 itakayowasaidia katika shughuli za kiuchumi kupitia ujasiriamali.

Mikopo hiyo yenye riba nafuu imetolewa na Mbunge wa Musoma Mjini mkoani Mara kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Vedastus Mathayo, ikiwa ni utekelezaji wa moja ya ahadi alizozitoa kwa wananchi wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani uliofanyika Oktoba 25, 2015. 


Wakati wa kampeni hizo, mwanasiasa huyo aliahidi kutoa shilingi milioni 200 kwa ajili ya kuwasaidia wanawake na milioni 50 za kuwawezesha vijana kiuchumi.

“Nimeanza utekelezaji wa ahadi zangu na hili suala la mikopo kwa akinamama wa daraja la chini nimelikamilisha kama nilivyoahidi wakati wa kampeni zangu kuelekea uchaguzi mkuu uliopita wa mwaka jana na ndiyo maana nimetoa milioni 200 kuwasaidia wanawake katika shughuli za ujasiriamali,” anasema Mathayo.

“Katikati ya mwezi huu wa Januari mtakumbuka nilizungumza na wenyeviti wa mitaa 73 ya Jimbo la Musoma Mjini na kuwapa jukumu la kusajili vikundi vya wanawake watakaowezeshwa fedha hizo. Nawapongeza kwa kuitikia mara moja zoezi hilo na tayari wanawake wameanza kupokea mikopo yao ya Sh 250,000 kwa kila kikundi cha watu 5 huku wakitakiwa kurejesha mikopo yao kwa riba ya asilimia mbili tu,” anasema.

Anasema, wakati anatoa ahadi hiyo ilikuwa si kutafuta kura pekee, alikuwa na dhamira ya kuwasaidia wananchi kupitia shughuli zao za ujasiriamali ili waweze kuwa na uchumi bora na kuondokana na umasikini unaowakabili kutokana na sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na ukosefu wa mitaji. 

Mathayo anasema, hahitaji kurudishiwa fedha hizo, ziwe na mpango mzuri ambao utaweza kuwawezesha wananchi kuzitumia kwa lengo la kuongeza kipato kwa kufanya ujasiriamali na si kuzitumia kwa njia isiyofaa.

Anasema, mikopo hiyo itakuwa inarejeshwa kwa lengo la kuwawezesha wanawake ambao hawajapata fursa hiyo nao waweze kukopeshwa. “Nimetoa fedha hizi kama ruzuku katika kuwasaidia wananchi wangu wa Jimbo la Musoma mjini, niliahidi na nimetekeleza na kinachohitajika ni usimamizi kuona fedha hizi zinatumika kuwasaidia na watu walioteuliwa kufanya zoezi la utoaji wa fedha wahakikishe fedha zinapotolewa ziende zikafanye kazi za kujenga uchumi,” anasema Mathayo.

Mbunge huyo anasema amekubaliana na uongozi wa benki Kata ya Imara (SACCOS) iliyopo Musoma Mjini kwa kushirikiana na watu wawili aliowateua kuweza kuweka mipango endelevu itakayoweza kuwasimamia wananchi kuzitumia fedha hizo kwa kuinua kiwango chao kiuchumi. 

Mwenyekiti wa Benki Kata hiyo, Boniphace Ndengo anasema wanachokifanya sasa ni utoaji wa elimu ya ujasiriamali kwa wananchi kabla ya kuwakabidhi fedha.

Anasema, lengo la elimu hiyo ni kuwaandaa kisaikolojia kuhusu umuhimu wa kukopa na jinsi ya kurejesha mikopo yao kwa wakati sambamba na jinsi ya kuitumia kwa malengo yaliyokusudiwa na si vinginevyo. 

Ndengo anasema, umewekwa utaratibu wa kurahisisha upatikanaji wa fedha hizo kupitia wenyeviti wa mitaa hivyo wanawake wafike kwenye ofisi za serikali za mitaa na kuanza taratibu za kujiunga kwenye vikundi.

Mkazi wa kata ya Nyasho, Kulwa Biseko ni miongoni mwa wanawake ambao tayari wamenufaika na mikopo hiyo waliyoichukua wiki iliyopita. 

Anamshukuru Mbunge Mathayo kwa kutekeleza ahadi yake kwa haraka na kutekeleza kwa vitendo Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2010-2015. Ibara ya 76 ya Ilani hiyo inaielekeza serikali kufufua kwa nguvu zote elimu yenye manufaa ya watu wazima nchini kote ili masomo ya ujasiriamali, uwezeshaji, urasimishaji wa biashara, kilimo, ufugaji na uvuvi yaweze kutolewa kwa wananchi wengi.

“Moja ya sehemu ya ibara hiyo inazungumzia umuhimu wa elimu kutolewa kwa njia ya mafunzo yanayolenga katika kuutokomeza umasikini wa wananchi walio wengi. Hivyo mafunzo ya ujasiriamali tuliyopewa kabla ya kupata mikopo hii ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya CCM na tunampongeza kwa dhati Mbunge wetu kuanza uongozi wake kwa kutekeleza falsafa ya Rais Magufuli ya Hapa ni Kazi Tu,” anasema Biseko.

Anaiomba serikali kutekeleza kwa vitendo Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015 -2020 kwa kuliangalia kundi kubwa la masikini lililo katika maisha ya chini kama ilivyobainishwa katika ibara ya 76 (b) kwa kuhamasisha uanzishwaji wa ushirika wa kuweka na kukopa (SACCOS na VICOBA), wa mazao, ujenzi, uvuvi, biashara na aina nyingine za ushirika ili wananchi wengi zaidi wajiunge na ushirika na wawezeshwe kimtaji kupanua shughuli zao za uzalishaji mali.
 
Anatoa mwito kwa viongozi wengine kuiga mfano wa Mbunge Mathayo aliyetoa fedha kutoka kwenye kipato chake na kuwasaidia wanawake Musoma Mjini wajikomboe kiuchumi. Anaiomba Serikali ya Awamu ya Tano kukuza mifuko ya uwezeshaji, kuboresha usimamizi na taratibu za kutoa mikopo ya riba nafuu ili walengwa wengi zaidi waweze kunufaika.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni